Social Icons

Alhamisi, 15 Mei 2014

NYOTA WA TANZANIA, MBWANA SAMATTA NA THOMAS ULIMWENGU KUTUA DAR..


RAIS wa shirikisho la soka nchini Tanzania, Jamal Malinzi imepigana kiume kuwasiliana na mwenyekiti na mmiliki wa klabu ya TP Mazembe, Moise Katumbi na taarifa njema juu ya mawasiliano hayo ni kwamba washambuliaji wawili wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta na Thomas Ulimwengu watawasili jumamosi mchana kwa ajili ya mchezo wa jumapili.
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya TFF zinaeleza kuwa Rais Malinzi amethibitisha ujio wa wanandinga hao tegemeo kwa Taifa stars na kuibua matumaini ya Taifa stars kufanya vizuri kwasababu Samatta na Ulimwengu ni wachezaji mahiri zaidi kwa sasa.
Nyota hao wawili watatumiwa kwa mara ya kwanza na kocha wa Taifa stars, Mart Nooij katika mechi ya raundi ya awali kuwania kufuzu fainali za mataifa ya Afrika mwakani nchini Morocco dhidi ya Zimbabwe kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam.
TP Mazembe aliwazuia wachezaji hao kuja Tanzania kwasababu wanawahitaji katika michezo ya makundi ya ligi ya mabingwa barani Afrika.
Matajiri hao wa DRC walipo kundi A wanatarajia kucheza mechi ya kwanza dhidi ya El Hilal Omduran siku ya ijumaa mjini Khartoum nchini Sudan, hivyo baada ya mechi hiyo wachezaji hao wa Tanzania watatua nchini jumamosi na kucheza mechi siku ya jumapili.
Hata hivyo baada ya mechi hiyo watakwea pipa kuelekea Lubumbashi DRC tayari kwa maandalizi ya mechi ya pili dhidi ya mahasimu wao AS Vita mei 25 mwaka huu.
Baada ya mechi hiyo na AS Vita ambapo wiki iliyopita walikutana nao katika mchezo wa mwisho wa ligi kuu ya DRC na kushuhudia vurugu kubwa ziliosababisha watu zaidi ya 15 kupoteza maisha, Samatta na Ulimwengu wataweza kupata nafasi ya kucheza mechi ya marudiano na Zimbabwe mjini Harare.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

 
 
Blogger Templates