Social Icons

Alhamisi, 31 Julai 2014

RAIS KIKWETE ATOA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KUFUATIA AJALI ILIYOTOKEA PANDAMBILI MKOANI DODOMA


THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

Telephone: 255-22-2114512, 2116898
Website : www.ikulu.go.tz              

Fax: 255-22-2113425



PRESIDENT’S OFFICE,
      STATE HOUSE,
              1 BARACK OBAMA ROAD,  
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Rehema Nchimbi kufuatia ajali iliyotokea tarehe 30 Julai, 2014 katika eneo la Pandambili, Wilayani Kongwa na kuua watu wapatao 18.
Katika ajali hiyo, watu 13 walifariki katika eneo la ajali, na majeruhi wapatao 56 walifikishwa hospitalini. Kati ya majeruhi hao hadi sasa waliolazwa ni 30 na wengine wameruhusiwa baada ya kupata matibabu.
Rais amemuomba Dkt. Nchimbi kumfikishia rambirambi zake za dhati kwa ndugu na jamaa waliopoteza wapendwa wao katika ajali hiyo, na kuwapa pole majeruhi wote na kuwatakia kupona haraka ili warejee kwenye shughuli zao za kila siku.
“ Natoa Pole za dhati kwa wale wote walioondokewa na wapendwa wao katika ajali hii na pia kuchukua nafasi hii kuwapa pole majeruhi wote na kuwaombea kupona haraka na kurudi katika shughuli zao za kila siku”.  Rais amesema katika salamu zake kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.

“Hakika ni jambo la kusikitisha sana kuondokewa na wananchi wetu katika ajali , natoa wito wangu kwa madereva wote na wote wanaotumia vyombo vya moto kuwa makini wanapokuwa barabarani “.  Rais amesema na kuongeza kuwa;  
“Kila dereva anaetumia chombo cha moto,  ana wajibu wa kulinda maisha yake na ya watumiaji wengine kwa kuwa makini na muangalifu awapo barabarani, kwani ajali hizi zinarudisha nyuma maendeleo ya taifa na ya wananchi kwa ujumla” Rais amesema na kuvitaka vyombo vya ulinzi na usalama barabarani kutolegeza kamba katika kuwachukulia hatua madereva wasio makini na wazembe wakati wote”.Rais amesisitiza.
Taarifa kutoka Mkoani Dodoma zinasema ajali hiyo ya jana (30 Julai, 2014) ilisababishwa na Lori  ambalo lilitaka kupita lori jingine na hivyo kwenda kugongana uso kwa uso na Basi la Moro Best lililokuwa likitokea Mpwapwa kuelekea Dar es Salaam.

……Mwisho……

Imetolewa na;
Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi,
Ikulu – Dar es Salaam.
30 Julai, 2014

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

 
 
Blogger Templates