Social Icons

Ijumaa, 20 Septemba 2013

SHAHIDI AFARIKI DUNIA MAHAKAMANI AKITOA USHAHIDI

Katika hali isiyo ya kawaida, mkazi wa Kijiji cha Lorwe Kata ya Nyahongo Shirati, wilayani Rorya, mkoani Mara, Charles Warito (38), ambaye ni shahidi wa mlalamikaji katika Kesi ya kudhuru mwili kwa kujeruhiwa vibaya kwa kukatwa mkono na kusababisha ulemavu amefariki dunia, wakati akitoa ushahidi.

Warito alikutwa na umauti huo akiwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Tarime mbele ya Jaji G. Ndika anayesikiliza kesi katika Wilaya za Tarime na Rorya.

Tukio hilo la kusikitisha lilitokea jana mchana baada ya Mwanasheria wa Serikali, Mayega na Mwendesha Mashitaka wa Polisi Inspekta George Lutonja walimwita kuingia Kizimbani tayari kutoa ushahidi.

Shahidi huyo alianza kutoa ushahidi wake na alieleza kushambuliwa kwa kukatwa mapanga na mtuhumiwa Kichohe Kichere ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Omoche Kata hiyo ya Nyahongo Shirati Januari 26, mwaka 2008 na kutokana na majeraha aliyoyapata kwa kukatwa mkono na mwili wake ulianza kupooza na kulemaa upande wa kulia ambao mkono ulikatwa

Alipoanza kujibu maswali kutoka kwa wakili wa mtuhumiwa mara alianza kulegea na kuishiwa nguvu na kuanguka kizimbani na kuzimia hali iliyofanya Mahakama hiyo Kusitisha Kusikiliza kesi na shahidi huyo kukimbizwa Hospitali ya Wilaya kupatiwa matibabu na alifariki kabla ya kupatiwa matibabu.

Mtuhumiwa katika kesi hiyo akiondoka haraka mahakamani hapo huku ndugu wa marehemu aliyejitambulisha kwa jina Otieno Rada alisema: "Nimesikitishwa na kifo hiki cha ndugu yangu Charles Joseph kwani majeraha hayo aliyoyapata ya kukatwa mkono na Kichere yalisababisha alemae mkono na kuanza kupooza na yamechangia kifo chake."

Mwili wa marehemu Charles umehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya Tarime ukisubili kuchukuliwa na ndugu zake kutoka Kijiji cha Lorwe Kata ya Nyahongo Shirati kwa maziko

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

 
 
Blogger Templates