Social Icons

Ijumaa, 27 Desemba 2013

RAGE ANENA.............Yanga haitufungi hadi tuhujumiane.


Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage

Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage ametoa kali baada ya kuifananisha timu ya Yanga na kikosi cha vijana wa Simba wenye umri chini ya miaka 20 (Simba B).

Akizungumza katika kipindi cha 'Hot Mix' kilichorushwa na EATV juzi jioni, Rage alisema kikosi cha Yanga kwa sasa ni sawa na Simba B, hivyo hakina uwezo wa kuifunga Simba.

"Yanga ni Simba B, itawachukua muda mregu sana kuja kutufunga. Wamejaza wachezaji wengi waliotoka kwetu (Simba) ambao lazima walipe fadhila kutokana na mazuri ambayo Simba iliwafanyia," alisema Rage.

"Kwa sasa Simba inaweza kufungwa na Yanga pale tu mmoja ama baadhi wa viongozi wetu wataamua kuihujumu timu yetu. Hawana uwezo wa kutufunga pasipo sisi (Simba) wenyewe kuhujumiana," alisema zaidi Rage.

Aidha, Rage alitumia muda huo kujibu hoja 'maiti' za 'waasi' wa Simba waliokuwa wakidai kwamba hajahusika hata kidogo katika kufanikisha ushindi wa timu yao dhidi ya Yanga Jumamosi.

"Kuna vitu visivyo na maana vinazungumzwa juu yangu. Naambiwa sijashiriki katika kufanikisha ushindi dhidi ya Yanga. Mchezaji aliyefunga bao la tatu (kiungo Awadh Juma) nilimsajili nyumbani kwangu na ndiye aliyechangia pia bao la kwanza," alisema.

Mbunge huyo wa Tabora Mjini (CCM) alibainisha kuwa watu wanaompinga wanasumbuliwa na ukata wa fedha, hivyo wanatafuta namna ya kumng'oa madarakani ili wahujumu mali za klabu hiyo.

"Wanasumbuliwa na njaa, ni njaa tu inawasumbua hao. Zipo njia sahihi za kikatiba za kuutoa madarakani uongozi. Wasubiri uchaguzi mkuu wa Simba," alisema kiongozi huyo anayesifika kwa lugha ya vijembe.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

 
 
Blogger Templates